5/20/2018

Kanisa la Mwenyezi Mungu | Sisitiza Zaidi Kwa Uhalisia

Kanisa la Mwenyezi Mungu | Sisitiza Zaidi Kwa Uhalisia

Mwenyezi Mungu alisema, Kila mtu ana uwezekano wa kukamilishwa na Mungu, kwa hiyo kila mtu anapaswa kuelewa ni huduma gani kwa Mungu itakayofaa zaidi makusudi ya Mungu. Watu wengi hawajui kumwamini Mungu humaanisha nini na hawajui chochote kwa nini wanapaswa kumwamini Mungu. Yaani, watu wengi sana hawana ufahamu wa kazi ya Mungu au lengo la mpango wa usimamizi wa Mungu. Hadi leo, watu wengi sana bado wanadhani kumwamini Mungu kunahusu kwenda mbinguni na roho zao kuokolewa. Bado hawajui chochote kuhusu umuhimu mahususi wa kumwamini Mungu, na aidha hawana ufahamu wowote wa kazi muhimu kabisa ya Mungu katika mpango Wake wa usimamizi. Kwa aina zote za sababu zao binafsi, watu hawavutiwi na kazi ya Mungu na hawatafakari juu ya makusudi ya Mungu au mpango wa Mungu wa usimamizi. Kama watu binafsi katika mkondo huu, kila mtu anapaswa kujua lengo la Mungu la mpango mzima wa usimamizi ni nini, ukweli ambao Mungu tayari amekwishatimiza, kwa nini Mungu amelichagua kundi hili la watu, malengo yake na umuhimu wake ni upi, na Mungu anataka kupata nini katika kundi hili. Katika nchi ya joka kuu jekundu, Mungu ameweza kuinua kundi hilo la watu wasioonekana kwa urahisi, na Ameendelea kufanya kazi hadi sasa, Akijaribu na kukamilisha wao kwa kila namna, Akizungumza maneno yasiyohesabika, Akifanya kazi kubwa na kutuma vitu vingi vya kuhudumu. Kutokana na Mungu kukamilisha kazi kubwa kiasi hicho, inaweza kuonekana kwamba umuhimu wa kazi ya Mungu ni mkubwa sana. Bado hamuwezi kuielewa kabisa. Kwa hiyo, msiichukulie kazi ambayo Mungu amefanya kwenu kama suala dogo; hiki si kitu kidogo. Kile tu ambacho Mungu amewaonyesha leo kinawatosha kutafakari na kukielewa. Ikiwa tu mnaelewa kwa kweli na kwa kina ndipo mtaweza kupata uzoefu wa kina zaidi na kupiga hatua katika maisha yenu. Kile ambacho watu wanakielewa na kukifanya sasa ni kidogo sana na hakiwezi kukidhi kikamilifu makusudi ya Mungu. Huu ni upungufu wa wanadamu na kushindwa kutimiza wajibu wao. Hii ndiyo maana matokeo ambayo yangepaswa kufikiwa bado hayajafikiwa. Roho Mtakatifu hawezi kufanya kazi kwa watu wengi kwa sababu wana ufahamu wa chini wa kazi ya Mungu na hawako tayari kuichukulia kazi ya nyumba ya Mungu kama kitu fulani cha thamani. Siku zote wanafanya vitu kwa namna isiyo ya dhati ili kuishi, au kuiga kile ambacho watu wengi sana wanafanya, au kuwaonyesha watu tu kwamba na wao "wanafanya kazi." Leo, kila mtu katika mkondo huu atakumbuka iwapo kile umefanya ndicho chote ambacho ungeweza kufanya, na iwapo umeweka jitihada zako zote. Watu hawajatimiza majukumu yao kabisa. Si kwamba Roho Mtakatifu hafanyi kazi Yake bali ni kwamba watu hawafanyi kazi yao, inafanya isiwezekane Roho Mtakatifu kufanya kazi Yake. Mungu amemaliza kuonyesha maneno Yake, lakini hawajaenda kwa kasi sawa kabisa, na wamebaki nyuma kabisa, wasiweze kukaa karibu na kila hatua, wasiweze kuzifuata nyayo za Mwana Kondoo kwa ukaribu. Kile ambacho walipaswa kukitii hawajakitii; kile ambacho walipaswa kukitenda hawajakitia katika vitendo; kile ambacho walipaswa kukiomba hawajakiomba; kile ambacho walipaswa kukiacha hawajakiacha. Bado hawajafanya kitu chochote kati ya hivi. Kwa hiyo, mazungumzo haya ya kwenda kwenye dhifa ni maneno matupu na hayana maana kabisa. Yapo katika fikra za watu tu. Inaweza kusemwa kamba hadi sasa watu hawajatimiza majukumu yao kabisa. Kila kitu kinategemea Mungu kufanya na kusema vitu Yeye Mwenyewe, wakati kazi ya watu kwa kweli imekuwa ndogo sana. Wote ni taka isiyokuwa na maana ambao hawajui jinsi ya kupatana na Mungu. Mungu amezungumza mamia ya maelfu ya maneno, lakini watu hawajayaweka katika vitendo kabisa, kuanzia kunyima mwili, kuacha dhana, kuwa watiifu katika mambo yote, kukuza ufahamu na kupata umaizi wakati huohuo, kuachana na hadhi za watu katika mioyo yao, kuondoa sanamu ambazo zinamiliki mioyo yao, kuasi dhidi ya makusudi binafsi ambayo si sahihi, kutofanya vitendo kulingana na mihemko yao, kufanya mambo kwa haki bila ubaguzi, kufikiri zaidi juu ya maslahi ya Mungu na ushawishi wao kwa wengine wanapozungumza, kufanya mambo mengi yanayonufaisha kazi ya Mungu, kukumbuka kunufaisha nyumba ya Mungu katika yote wanayofanya, kutoruhusu mihemko yao kuamua tabia zao, kuacha yale ambayo yanapendeza miili yao, kuondoa dhana za zamani za ubinafsi, na kadhalika. Kwa kweli watu wanafahamu baadhi ya mambo katika maneno haya yote juu ya kile ambacho Mungu anahitaji kutoka kwao, lakini hawako tayari kuyaweka katika vitendo. Ni kwa namna gani nyingine ambayo Mungu anaweza kufanya kazi na kuwashawishi? Ni kwa jinsi gani waasi machoni pa Mungu bado wana ujasiri wa kuchukua maneno ya Mungu na kuyastahi? Wanawezaje kuwa na ujasiri wa kula chakula cha Mungu? Dhamiri ya mwanadamu ipo wapi? Hawajatimiza wajibu mdogo kabisa waliopaswa kutimiza, kwa hiyo kuzungumza juu ya kufanya yote wawezayo ni hoja isiyokuwa na maana. Je, wao si watu wa njozi tu? Hakuwezi kuwa na mazungumzo ya uhalisia bila matendo. Huo ni ukweli wa wazi kabisa!
Mnapaswa kuwa mnajifunza masomo zaidi ya uhalisia sasa. Hakuna haja ya hayo mazungumzo tupu, yenye kuvutia ambayo watu wanayastahi. Linapokuja suala la kuzungumza kuhusu maarifa, kila mtu yupo juu kuliko anayefuata, lakini bado hawana njia ya kufanya vitendo. Ni wangapi wameweka kitu chochote katika vitendo? Ni wangapi wamejifunza masomo halisi? Ni nani anaweza kufanya ushirika kuhusu uhalisia? Kuweza kuzungumza juu ya maarifa ya maneno ya Mungu si sawa na kimo chako halisi. Huonyesha tu umezaliwa ukiwa na akili na ni mwenye karama. Bado inakuwa haina maana ikiwa huwezi kuonyesha njia, na wewe ni taka tu isiyokuwa na maana! Je, hujifanyi tu ikiwa huwezi kusema chochote kuhusu njia halisi ya kufanya vitendo? Je hujifanyi ikiwa huwezi kutoa uzoefu wako mwenyewe halisi kwa wengine, na hivyo kuwapa masomo ambayo wanaweza kujifunza kwayo au njia ya kufanya vitendo? Je, wewe si bandia tu? Una thamani gani? Mtu kama huyo angeweza tu kushikilia sehemu ya kuwa "mvumbuzi wa nadharia ya ujamaa," si "mchangiaji wa kuleta ujamaa." Kutokuwa na uhalisia ni kutokuwa na ukweli. Kutokuwa na uhalisia ni kutokuwa na thamani. Kutokuwa na uhalisia ni kukosa uhai. Kutokuwa na uhalisia ni "kuwa na fikra za Ki-Marx-Lenini," bila thamani kama marejeo. Ninamsihi kila mtu kufunga mdomo kuhusu nadharia na kuzungumzia kitu ambacho ni halisi, kitu ambacho ni cha kweli na thabiti, kujifunza baadhi ya "sanaa za kisasa," kuzungumza juu ya kitu ambacho ni halisi, kuchangia uhalisia kiasi, na kuwa na roho ya kujitoa. Ukabili uhalisia unapozungumza na usijiingize katika mazungumzo yasiyokuwa na uhalisia na yaliyoongezwa chumvi ili kuwafurahisha watu au ili waweze kukufikiria kwa namna tofauti. Thamani yake ni nini? Kuna maana gani katika kuamsha shauku za watu kwa ajili yako? Kuwa "stadi" katika usemi wako, tenda haki katika matendo yako, kuwa mwenye busara katika kazi yako, kuwa mwenye uhalisia katika kuwahutubia watu, kumbuka kuinufaisha nyumba ya Mungu katika kila tendo, wacha dhamiri yako iongoze hisia zako, usilipize wema kwa chuki, au kutokuwa na shukrani kwa wema, na usiwe mnafiki, usije ukawa na "ushawishi mbaya." Unapokula na kunywa maneno ya Mungu, yahusishe na uhalisia, na unapowasiliana, zungumza zaidi kuhusu mambo ya uhalisia na usijikweze—Mungu hukataa hilo. Kuwa mvumilivu na mstahimilivu zaidi, fanya mazoezi zaidi ya kukubali, kuwa mkarimu na wazi kwa watu, na jifunze kutoka kwa "roho ya waziri mkuu."[a] Unapokuwa na mawazo ambayo si mazuri, fanya mazoezi zaidi ya kunyima mwili zaidi. Unapofanya kazi, zungumza zaidi kuhusu njia halisi na usiwe na majivuno sana vinginevyo itakuwa zaidi ya upeo wa watu. Starehe kidogo, mchango zaidi—onyesha roho yako ya kujitolea isiyo ya ubinafsi. Fikirieni zaidi makusudi ya Mungu, sikilizeni zaidi dhamiri zenu, na kumbuka zaidi na msisahau jinsi ambavyo Mungu huwaonya kila siku kwa kuwajali. Soma "shajara ya mwaka ya zamani" mara kwa mara. Omba zaidi na shiriki mara kwa mara. Usiendelee kuwa mtu wa kuboronga, bali kuwa na busara zaidi na pata umaizi. Mkono wa dhambi unaponyooshwa, urudishe nyuma na usiuache utandae zaidi. Haina maana! Mnachokipata kutoka kwa Mungu si chochote bali laana; kuweni waangalifu. Wacheni mioyo yenu iwe na huruma kwa wengine na siku zote msiwapige kwa silaha mkononi. Toeni zaidi na zungumzeni zaidi kuhusu maisha, mkiwa na roho ya kuwasaidia wengine. Tendeni zaidi na kusema kidogo. Tia zaidi katika vitendo na kidogo katika utafiti na uchambuzi. Mshawishiwe zaidi na Roho Mtakatifu, na mpeni Mungu fursa zaidi ya kuwakamilisha. Ondoeni zaidi sifa za kibinadamu—bado kuna namna nyingi za kibinadamu za kufanya mambo. Matendo na tabia za juujuu bado zinachukiza kabisa. Ziondoeni zaidi. Hali zenu za akili bado zinachukiza sana. Zisahihisheni zaidi. Hadhi ambayo watu wanamiliki katika mioyo yenu bado ni kubwa sana. Mpatie Mungu hadhi zaidi na usiwe mtu usiyekuwa na akili. "Hekalu" kwanza ni la Mungu na halipaswi kumilikiwa na watu. Kwa ujumla, sisitiza zaidi haki na kidogo katika mihemko, na ni bora zaidi kuuondoa mwili; zungumza zaidi kuhusu uhalisia na kidogo kuhusu maarifa, na ni bora zaidi kuwa kimya; zungumza zaidi juu ya njia ya vitendo na kwa kiasi kidogo mazungumzo ya kiburi yasiyokuwa na maana, na ni bora zaidi kuanza vitendo kuanzia sasa.
Matakwa ya Mungu kwa watu si ya juu sana. Ikiwa watu wataweka jitihada kidogo wataweza kupata "alama ya ufaulu." Kwa kweli, kufahamu, kujua, na kuukubali ukweli kunatatiza sana kuliko kuutenda ukweli; kuujua na kuukubali ukweli kunakuja baada ya kuutenda ukweli kwanza. Hii ndiyo hatua na njia ya kazi ya Roho Mtakatifu. Unawezaje kutoitii? Je, utaweza kuwa na kazi ya Roho Mtakatifu kwa kufanya mambo kwa namna yako? Je, Mungu hufanya kazi kwa kuzingatia matakwa yako, au baada ya wewe kulinganisha dhidi ya maneno ya Mungu? Haina maana ikiwa huwezi kuliona hili kwa uwazi. Kwa nini watu wengi sana wametumia jitihada nyingi kusoma maneno ya Mungu lakini wanakuwa tu na maarifa na hawawezi kusema kitu chochote kuhusu njia halisi baada ya hapo? Unadhani kwamba kuwa na maarifa ni sawa na kuwa na ukweli? Je, huo si mtazamo uliokanganywa? Unaweza kuzungumza maarifa mengi kama mchanga wa bahari, lakini hakuna yaliyo na njia ya kweli. Katika hili, je huwadanganyi watu? Je, wewe si mtu wa maneno matupu bila vitendo? Kutenda kwa namna hii ni hatari kwa watu! Kadri nadharia inavyokuwa ya juu, ndivyo inavyokosa uhalisia, na ndivyo inavyokosa uwezo wa kuwapeleka watu katika uhalisia; kadri nadharia inavyokuwa ya juu, ndivyo inavyokufanya kumuasi na kumpinga Mungu. Usizichukulie nadharia za kiwango cha juu kama hazina ya thamani; zina madhara, na hazina kazi yoyote! Pengine baadhi ya watu wanaweza kuzungumza juu ya nadharia za juu sana—lakini nadharia hizo hazina kitu chochote cha uhalisia, maana watu hawa hawajawa na uzoefu binafsi nazo, na kwa hiyo hawana njia ya kutenda. Watu kama hao hawawezi kumwongoza mwanadamu katika njia nzuri, na watawapotosha tu watu. Je, hii si hatari kwa watu? Kwa kiwango cha chini kabisa, unapaswa uweze kutatua shida za sasa na kuwaruhusu watu kupata kuingia; hii tu ndiyo inahesabika kama ibada, na baada ya hapo ndipo utakuwa na sifa za kufaa kumfanyia Mungu kazi. Siku zote usizungumze maneno mazuri, ya kibunifu, na usiwalazimishe watu kukutii wewe pamoja na vitendo vyako visivyofaa. Kufanya hivyo hakutaleta matokeo mazuri, na kutaongeza tu mkanganyiko wa watu. Kuwaongoza watu namna hii kutazalisha taratibu nyingi, ambazo zitafanya watu wakuchukie. Huu ndio udhaifu wa mwanadamu, na kwa kweli hauvumiliki. Kwa hiyo, zungumza zaidi juu ya matatizo yaliyopo sasa. Usichukulie uzoefu wa watu wengine kama mali binafsi na kuuleta kwa wengine ili wautambue. Wewe binafsi unapaswa kutafuta njia ya kutokea. Hiki ndicho kila mtu anapaswa kuweka katika vitendo.
Ikiwa kile unachosema kinaweza kuwapatia watu njia ya kutembea, basi hiyo ni sawa na wewe kuwa na uhalisia. Haijalishi kile unachosema, ni lazima uwalete watu katika vitendo na kuwapatia njia wanayoweza kuifuata. Si tu kuhusu kuifanya ili watu wapate maarifa, lakini muhimu zaidi, ni kuhusu kuwa na njia ya kutembea. Ili watu wamwamini Mungu, wanapaswa kutembea njia ambayo kwayo Mungu huwaongoza. Yaani, mchakato wa kumwamini Mungu ni mchakato wa kutembea kwenye njia ambayo kwayo Roho Mtakatifu hukuongoza. Vivyo hivyo, unapaswa kuwa na njia ambayo kwayo unaweza kutembea kwa vyovyote vile, na unapaswa kutembea kwenye njia ya kukamilishwa na Mungu. Usilitumie zaidi ya kiasi, na usijihusishe nayo sana. Ikiwa tu unatembea kwenye njia ambayo kwayo Mungu hukuongoza bila kusababisha mwingiliano ndipo unaweza kupokea kazi ya Roho Mtakatifu na kuwa na njia ya kuingia. Hili tu ndilo linahesabika kama la kufaa makusudi ya Mungu na kutimiza wajibu wa mwanadamu. Kama watu binafsi katika mkondo huu, kila mtu anapaswa kutimiza wajibu wake kwa usahihi, fanya zaidi ambayo watu wanapaswa kufanya, na usitende kwa lengo la kudhuru. Watu wanaotekeleza kazi wanapaswa kuweka maneno yao wazi, watu wanaofuata wanapaswa kusisitiza zaidi kuhimili ugumu na kutii, na kila mtu anapaswa kutunza nafasi yake na kutotoka nje ya mstari. Linapaswa lieleweke wazi katika moyo wa kila mtu namna ambavyo wanapaswa kutenda na kazi gani wanapaswa kutimiza. Chukua njia ambayo kwayo Roho Mtakatifu huongoza; usipotoke au kukosea. Mnapaswa kuiona kazi ya leo waziwazi. Kuingia katika mbinu ya kazi ya leo ndicho mnachopaswa kutenda. Ni kitu cha kwanza mnachopaswa kuingia. Msipoteze maneno zaidi kwenye mambo mengine. Kufanya kazi ya nyumba ya Mungu leo ni jukumu lenu, kuingia katika mbinu ya kazi ya leo ni wajibu wenu, na kutenda ukweli wa leo ni mzigo wenu.
Tanbihi:
a. Roho ya waziri mkuu: Ni msemo wa jadi wa Kichina ambao hutumika kuelezea mtu anayekubali kusikiliza mawazo ya wenzake japo si lazima akubaliane nayo na mkarimu.
kutoka kwa Neno Laonekana katika Mwili
Yaliyopendekezwa: Kuhusu Umeme wa Mashariki

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni